Dec 5, 2013

HISTORIA: Mandela tangu kuzaliwa hadi kufariki dunia, Pumzika kwa amani, 1918 - 2013


Mzee Nelson Mandela aliyefariki dunia usiku wa 05/12/2013, alizaliwa mwaka 1918 na hatimaye kuwa rais wa kwanza mzalendo wa Afrika Kusini baada ya kuongoza mapambano ya muda mrefu dhidi ya utawala wa kibaguzi wa makaburu.
Mandela ambaye nchini Afrika Kusini anajulikana kwa jina la MADIBA, alifungwa jela kwa kipindi cha miaka 27 katika kisiwa cha Robben kutokana na harakati zake za kupinga ubaguzi wa rangi na kupigania uhuru wa nchi ya Afrika Kusini.
Baada ya kuachiwa kwake huru Februari 11 mwaka 1990 alihamasisha siasa za amani na suluhu, suala ambalo lilirahisisha mchakato wa kuiondoa Afrika Kusini katika utawala wa wazungu wachache na kuelekea kwenye demokrasia.
Pia Nchini Afrika Kusini Nelson Mandela anajulikana kwa jina la TATA lenye maana ya BABA.
Katika kipindi chote cha miongo minne ya harakati zake za kisiasa Mzee Mandela ametunukiwa zaidi na tuzo 250 ikiwemo tuzo ya amani ya Nobel mwaka 1993.
PAMOJA NA HAYO.
Kutokana na mapambano yake dhidi ya ubaguzi wa rangi na kupigania uhuru wa Afrika Kusini nchi za Magharibi zilizokuwa zikiwaunga mkono makaburu wabaguzi zilimtambua Mandela kuwa ni gaidi.
Shujaa huyo wa Afrika aliwekwa kwenye orodha ya magaidi ya Marekani kwa miaka mingi na aliendelea kuwekwa kwenye orodha ya magaidi ya serikali ya Washington hata wakati alipokuwa Rais aliyechaguliwa na wananchi.
Mandela aliondolewa kwenye orodha ya magaidi ya Marekani mwaka 2008. Kuwekwa jina la mpigania uhuru mkubwa wa Afrika katika orodha ya magaidi ya Marekani kunafichua na kuweka wazi maana ya ugaidi katika kamusi ya kisiasa ya nchi hizo za Magharibi.